RIADHA HARD TALK 2014: RT yabariki mjadala wa riadha Holili


SHIRIKISHO la Riadha Tanzania (RT), limeimwagia sifa klabu ya Holili Youth Athletics (HYAC) iliyoko Holili, Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro kwa kuandaa mjadala wa kujadili changamoto zinazokabili mchezo wa riadha nchini.

Mjadala huo utafanyika kesho katika ukumbi wa Moshi Club ulioko pembezoni mwa mji wa Moshi, mkoani Kilimanjaro, ambapo zaidi ya wadau 100 wanatarajiwa kushiriki.

Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu, Katibu Mkuu wa RT, Suleiman Nyambui, alisema shirikisho lake limetoa baraka zote kwa klabu hiyo na mjadala huo na kutoa wito kwa wanamichezo wenye nia njema na maendeleo ya riadha kujitokeza kwa wingi kushiriki.

Nyambui, aliwataka wadau wa riadha waelewe kwamba mjadala huo haujaandaliwa kwa ajili ya kusutana bali kuunganisha akili kuangalia mbinu za kutatua changamoto zinazokabili michezo hapa nchini.

“Watanzania na wapenzi wa riadha waelewe kwamba mjadala huu utalenga kujadili matatizo yetu kama taifa katika riadha na kuangalia mbele, tusifike mahali tukaanza kutumia mjadala huo kama uwanja wa mapambano,” alisema Nyambui.

Wakati huo huo, Kampuni ya vinywaji baridi ya Bonite Bottlers, imetoa msaada wa vinywaji kwa klabu hiyo vitakavyotumika wakati wa mjadala huo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Meneja Mauzo wa Bonite, Christopher Loiruki, alisema kampuni yake itaendelea kuunga mkono jitihada zote zinazofanyika kuinua michezo hapa nchini.

“Sisi kama wadau wa michezo kila mara tutakuwa mstari wa mbele kusaidia jitihada za kuinua michezo hapa nchini, kwa muktadha huo leo tunatoa kreti za soda na maji kwa ajili ya mjadala wenu,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Holili, Domician Rwezaura, alisema lengo la kuandaa mjadala huo ni kukusanya maoni ya wadau wa mchezo huo kuhusu nini kifanyike kuufufua na kuurudishia hadhi yake kama ilivyokuwa katika miaka ya nyuma.

“Tumeamua kuandaa mjadala huu sio kujionyesha au kuomba msaada, lengo letu ni kutafuta mawazo ya wadau wa riadha juu ya nini kifanyike kufufua mchezo wa riadha Tanzania na kuirudisha kule ilikokuwa miaka ya 70,” alisema Rwezaura.

CHANZO: Tanzania Daima

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga