Glasgow: Emiliani anyukwa, Ikangaa, Bazil leo

Dar es Salaam. Bondia Emiliani Patrick ameendeleza rekodi mbaya ya Tanzania kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola baada ya jana kupokea kipigo kutoka kwa Mganda Bashir Nasir.
Bondia Emiliani Patrick aliaga kwenye michezo hiyo baada ya kuruhusu kipigo cha pointi za majaji 2-1 dhidi ya Mganda huyo.
Katika pambano hilo, Emiliani alipata matokeo ya pointi 28-29 raundi ya kwanza, 27-30 na raundi ya mwisho aliongoza kwa pointi 29-28.
Kwa matokeo hayo sasa mategemeo ya Tanzania walau kutwaa medali kwenye michezo hiyo yamesalia kwa wanamichezo watatu.
Hadi jana, wanamichezo 36 wa Tanzania walioshiriki ngumi, riadha, judo, mpira wa meza, kunyanyua vitu vizito, kuogelea na baiskeli walikuwa tayari wameondoshwa kwenye mashindano hayo.
Tegemeo pekee kwa Tanzania lipo kwa wanariadha, Dotto Ikangaa na Bazil John watakaochuana katika mbio za kati za mita 1,500 na bondia, Hamad Furahisha aliyetarajiwa kuzichapa jana usiku.
Kwa mujibu wa meneja wa timu za Tanzania kwenye michezo hiyo, Muharami Mchume, wanariadha Ikangaa na John watachuana katika mchujo kutafuta tiketi ya kuingia fainali kwenye mbio hizo zitakazofanyika kwenye Uwanja wa Hampden Park jijini Glasgow.
“Furahisha atazichapa na Paddy Barnes wa Ireland Kaskazini jioni hii ‘jana’ kwenye ukumbi wa SECC 4A katika pambano la uzani wa light fly akishinda anaingia robo fainali,” alisema
Juzi jioni kwenye Uwanja wa Hampden Park, Watanzania, Fabian Sulle na Wilbaldo Malley walishindwa kufurukuta katika fainali ya mbio za mita 5,000 na kushuhudia Caleb Ndiku wa Kenya akiibuka kinara baada ya kukimbia kwa dakika 13:12:07.
Isiah Koech wa Kenya aliyekimbia kwa dakika 13:14:06 alimaliza wa pili huku Zane Robertson wa New Zealand akihitimisha tatu bora baada ya kukimbia kwa dakika 13:16:52.
Katika mbio hizo zilizoshirikisha wanaraidha 24, Sulle alimaliza kwenye nafasi ya 14 akiwa amekimbia kwa dakika 13: 44:65 na Malley alimaliza kwenye nafasi ya 18 akitumia dakika 14:10:92.
Kwenye ngumi, bondia Gaudence Pius ameshindwa kutamba mbele ya Sean Duffy wa  Ireland Kaskazini na kuruhusu kipigo cha pointi za majaji 2-1 kwenye pambano lake la kutafuta tiketi ya kucheza robo fainali kwenye ukumbi wa SECC 4A.

Jaji wa kwanza alimpa ushindi wa pointi 29-28 kwa Pius, jaji wa pili 28-29 na jaji wa tatu alimpa Pius pointi 28-29. Tanzania imetwaa medali sita za dhahabu, tisa za fedha idadi sawa na medali za shaba katika Michezo ya Jumuiya Madola tangu 1962.
Michezo mingine ya Tanzania inayoshindanishwa kwenye madola ni riadha, ngumi, baiskeli na kunyanyua vitu vizito.

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga