KAULI YA NYAMBUI NI KIPIMO TOSHA CHA UDHAIFU WA UZALENDO WETU

Suleiman Nyambui / Mtanzania asiyejali sheria wala uzalendo
KATI ya vipindi vya michezo redioni ambavyo hunipita kwa nadra sana ni kile cha Radio One Stereo. Siku chache zilizopita, nilikuwa nikifuatilia namna Maulid Kitenge alivyokuwa akimhoji Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Tanzania (RT), Selemani Mujaya Nyambui.

Kitenge alikuwa akitaka kujua sababu ya timu ya Tanzania iliyoshiriki michuano ya Jumuiya ya Madola kurejea nyumbani bila ya hata kipande cha medali.

Nyambui ambaye katika sauti yake unaweza kubaini mengi, alizungumza mambo ya ajabu ambayo hauwezi kutarajia kiongozi au mwanamichezo mwenye sifa yake anaweza kuzungumzia.

Mwanariadha huyo wa zamani ambaye unaweza kumwita ni kati ya mashujaa waliowahi kuchukua medali na kuileta nyumbani kupitia michuano ya Olimpiki, alikuwa akizungumza sawa na mtu aliyekuwa hayuko vizuri, labda kwa uchovu au ni yule asiyejali tu.

Wakati Kitenge akieleza alitaka kujua kwa nini timu hiyo haikuleta medali, Nyambui hakufafanua lolote zaidi ya kuhoji vipi Taifa Stars nayo mbona imefungwa na Msumbiji na kurejea nyumbani mikono mitupu!

Hata aliposisitiziwa kwamba suala la soka halimhusu na alipaswa kujibu lile linalomhusu, akasema anashangazwa na watu kuhoji medali wakati hawajui hata muda mzuri waliokimbia wanariadha waliokwenda Glasgow, Scotland na hicho ndiyo kitu cha kujivunia.

Huyo ni mwanariadha nyota wa zamani wa nchini, kiongozi wa sasa wa mchezo wa riadha ambaye anadiriki kuzungumza pumba tena akionyesha hajali na badala ya kufafanua anachoelezwa, yeye anakwenda kuhoji vipi wengine pia wamefanya vibaya!
Majibu ya Nyambui yanathibitisha kwamba mafanikio katika mchezo wa riadha sasa ni ndoto, labda hadi mambo mawili yatokee.
Kwanza Nyambui aondoke kwenye uongozi wa mchezo huo au soka warudi na kombe nyumbani baada ya kushinda nje, basi Nyambui ataongeza juhudi kuwajibu.

Anachokisema anaonyesha hajali kwa kuwa soka hawajashinda, wangeshinda huenda angesikia wivu. Lakini kwa anachozungumza, inaonyesha wazi kiongozi huyo ni sehemu kubwa ya tatizo katika mchezo wa riadha.

Sijui wangapi walimsikiliza Nyambui, lakini kwa waliopata nafasi ya kumsikiliza ‘live’ sijui walitafakari vipi lakini mimi naweka wazi hisia zangu kwamba ingawa ni mwanariadha wa zamani, anaonyesha kiasi gani asivyo na uchungu na Tanzania kutofanya vizuri.

Huu ndiyo wakati mzuri na mwafaka wa wanamichezo au Watanzania kwa jumla kuanza kuhoji na kuwakemea watu kama akina Nyambui ambao wamejisahau na kugeuza vyama vya riadha kama mali yao huku wakiamini hakuna mtu anayeweza kuwahoji kutokana na kinachotokea.
Lazima tujue kwamba kizuri na kibaya, kinahusisha jina la nchi yetu Tanzania.

Tusiruhusu watu kama kina Nyambui wakaendelea kuzaliwa wengine ambao watakuwa kila kitu wanakichukulia kwa urahisi huku wakiona vyama wanavyoviongoza utafikiri ni mangi anayemiliki duka, hivyo wanaweza kuamua muda wa kufunga na kufungua.

Tunajua mamilioni ya fedha yamekuwa yakitolewa na mashirikisho ya fedha kwa ajili ya maandalizi ya michuano mbalimbali ya kimataifa ambayo mwisho wake hatufanyi vizuri.

Kama hiyo haitoshi, safari hii serikali kupitia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, ilitumia fedha za kodi ya Watanzania kwa ajili ya maandalizi ya timu hiyo ya Jumuiya ya Madola.

Sasa kuzungumza kama vile unazungumzia familia yako, bila ya kujua Watanzania wengine wanaumia vipi, si kitu sahihi.

Leo nakutumia salamu hizi Nyambui lakini nakuasa, kuna haja ya kuonyesha kiasi gani una uchungu na taifa lako na si kufurahia tu kusafiri na kulala kwenye hoteli nzuri halafu mnarudi mikono mitupu na maneno mengi ya kujidai yasiyokuwa na ustaarabu au kuonyesha upevu. Inaonyesha huwa mnajua mtarudi hamna kitu!

CHANZO: Gazeti la Champion


Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga