MICHEZO MADOLA: Makocha wajilipua

Makocha wa timu za Tanzania zilizoshiriki na kufanya vibaya kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola iliyomalizika nchini Scotland wamefunguka na kueleza masaibu yaliyozisibu timu zao.

Katika kile kinachoonyesha kuwa kimya kingi kina mshindo, mkuu makocha hao wameeleza mambo mazito ambayo ni vigumu kuyaamini, lakini  ndiyo yaliyozikumba timu za Tanzania. Mojawapo ni jambo ambalo ni hatari kiafya, aibu na fedheha,  likiwamo la mabondia kulazimika kupokezana vikinga ulimi, hali inayoweza kusababisha maradhi.
Mtaalam mmoja wa michezo, Dk Nassoro Matuzya alisema jana kuwa kubadilisha vikinga ulimi ni hatari na kiafya hairuhusiwi, kwani mdomo ni mojawapo ya sehemu zenye bakteria wengi katika mwili wa binadamu, jambo ambalo ni rahisi kuambukizana magonjwa.
“Wanaofanya hivyo wanapaswa kuwa na wataalam wa afya ili wawashauri kuhusu madhara yanayoweza kuwapata wanamichezo kwa kupewa vitu kama hivyo,” alisema na kuongeza kuwa kama kuna timu imewahi kufanya hivyo, wachezaji wake wapo hatarini kupata magonjwa ya kuambukiza yakiwamo ya kinywa.
 Kwa upande wao, wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti, kocha wa ngumi, Jonas Mwakipesile na mwenzake wa judo, Hamis Zaid walidai Serikali haisemi ukweli juu ya ushiriki  duni kwenye michezo hiyo huku mzigo wa lawama baada ya timu kurejea mikono mitupu wakitupiwa wao.
Makocha hao walisema, Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo imeshindwa kuwaambia ukweli Watanzania kuhusu kile kilichokuwa kinatendeka kwa timu zao kwenye michezo hiyo  iliyomalizika Agosti 3 nchini Scotland huku lawama zote zikipelekwa kwao (makocha) na wachezaji.
“Wizara  imechangia timu kufanya vibaya, tulifika Glasgow lakini hadi siku ya ufunguzi wa mashindano, timu hazina vifaa vya mashindano, wakati tuonaondoka nchini tuliambiwa tutapewa tukifika  huko. “Kilichofanyika tuliletea vikinga ulimi na protekta chache, tukaambiwa mabondia wapokezane kwani Serikali haina fedha, hatukuwa na namna zaidi ya kufanya hivyo, kuwaacha vijana wapokezane  vikinga ulimi hivyo, ilikuwa aibu,” alisema Mwakipesile.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi za Ridhaa (BFT), Makore Mashaga kwa upande wake alisema  wakati timu inaondoka ilikuwa chini ya Serikali, hivyo wao hawahusiki na madai kuwa walikuwa wakipokezana vikinga ulimi. “Sidhani kama Serikali ilishindwa kuwanunulia vikinga ulimi kwani kimoja kinauzwa  Sh10,000 hadi Sh20,000 kutokana na ubora, protekta moja ni  Sh40,000 mpaka Sh50,000 kama walikosa hiyo ni juu ya Serikali kwani ndiyo tuliikabidhi timu,” alisema.
Naye Hamis Zaid, ambaye aliondoka na timu ya judo alisema Serikali imechangia wao kufanya vibaya kwani ilishindwa kufanya majukumu yake kama Serikali kwenye michezo hiyo hali iliyowavunja moyo wachezaji wake. “Inashangaza, lawama zote tunatupiwa sisi makocha, lakini Serikali haitaki kusema ukweli nini kilikuwa  kinatendeka kule, tumecheza mashindano kwa kutumia vifaa vya kuazima, siku chache kabla ya mashindano kwisha ndipo wakatuletea vifaa ili vitusaidie nini,” alihoji.

Alisema walilazimika kuazima vifaa kwa waandaji kule Scotland, ambao kiutaratibu kama nchi ikiazima zaidi ya mara mbili kocha anapewa adhabu ya kugeuka mtazamaji na mchezaji anakwenda ulingoni peke yake, hivyo dhahama hiyo ilimkumba ambapo mchezaji wake, Amour Kombo kuingia ulingoni bila sapoti ya kocha. “Mchezaji wangu tegemeo, Ahmed Magogo aliondoshwa mashindanoni, hakucheza, sababu ni  kuchelewa kupima uzito, ukiuliza ni kwanini aliachwa Tanzania wakati wenzao wanaondoka sababu haijulikani, hii yote ni ubabaishaji,” alisema.
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo kutoka wizara ya Habari,  Utamaduni, Vijana  na Michezo, ambaye pia alikuwa mkuu wa msafara kwenye michezo hiyo, Leonard Thadeo alipoulizwa jana kuhusu madai hayo ya makocha alikataa kuzungumzia kilichotokea kwenye michezo hiyo. “Mimi siwezi kuzungumzia mambo ya Madola, sisi tuna utararibu wetu, sihitaji kuzungumza chochote kuhusu michezo hiyo kwenye vyombo vya habari,” alisema Thadeo.

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga