Viongozi wa michezo nchini ‘janga la Taifa’

Mhe.Dr.Fenella Mukangara / Waziri wa Michezo
Wakati wa utawala wa Baba wa Taifa, Marehemu Julius Kambarage Nyerere, Tanzania iliingia kwenye rekodi ya mataifa tishio barani Afrika katika michezo.
Wakati huo, wanamichezo wa taifa waliaminika kwa Watanzania kila waliposema wanakwenda kushindana nje ya nchi. Si kama Tanzania ilishushiwa muujiza bali ilitokana na namna viongozi wa Serikali na wale wa michezo wa wakati huo walivyotambua wajibu wao. Historia zinaonyesha namna michezo ilivyofanyika kwa mpangilio kuanzia ngazi za shule, kata, wilaya, mkoa na taifa, vipaji vilionekana na Taifa likafanya vizuri kimataifa.
Tanzania iling’ara kwenye mashindano ya Olimpiki, Jumuiya ya Madola na Afrika wakati huo kutokana na namna taifa lilivyotengeneza timu za ushindani kuanzia ngazi ya wilaya, mikoa na hata taifa hivyo kuwa na akiba ya vijana wengi wenye vipaji vya michezo. Tofauti na sasa ambapo kadri siku zinavyozidi kwenda ndivyo jahazi la michezo ya Tanzania linazidi kuzama, hakuna mchezo wenye afadhali kuanzia kwenye soka, riadha, ngumi, tenisi, kikapu, netiboli na michezo mingine mingi.
Bila shaka utaungana na mimi na kukubaliana nami kuwa michezo ya Tanzania sasa iko hoi. Wakati wowote kuanzia sasa chochote kinaweza kutokea, lakini cha kushangaza hakuna kiongozi hata mmoja wa michezo anayeonyesha kujali wala kuweweseka na hali hiyo. Kuanzia mamlaka ya juu iliyopewa dhamana ya kuongoza michezo yaani Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo na kurugenzi zake mpaka wale viongozi wa chini waliopewa dhamana ya kuongoza michezo, wote wanaonyesha kuridhika na hali iliyopo hivi sasa.
Inashangaza kweli kuona viongozi wa Chama cha Riadha (RT)wanasimama tena hadharani na kuzungumza kwamba chama hakina uwezo wa kufanya jambo la maendeleo huku kikidai Serikali kushindwa kuwasaidia. Pia Wizara inayohusika na michezo inasimama na kusema hakuna bajeti ya kusaidia michezo kwa kuwa Serikali haina fedha. Hivi kwa mvutano huu, viongozi hawa walitaka nani aje aionee huruma Tanzania na kuisaidia ili ifanikiwe katika michezo?, kama viongozi wa michezo hawana mikakati ya maendeleo wanategemea muujiza gani katika michezo ya Tanzania?.
Inashangaza Tanzania imebaki kuwa mtazamaji wakati nchi nyingine zikichukua medali kwenye mashindano ya kimataifa. Tumeshuhudia udhaifu wa timu zetu kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola, Olimpiki na hata dunia huku timu yetu ya soka ikitafuta kwa udi na uvumba nafasi ya kucheza angalau fainali za Mataifa ya Afrika bila mafanikio.
Tanzania ina wachezaji wengi wenye vipaji na uwezo mkubwa ingawa inaponzwa na mfumo wa uongozi katika sekta ya michezo. Ninapozungumzia mfumo wa uongozi katika sekta hii namaanisha kuanzia Wizarani, Baraza la Michezo la Taifa (BMT) hadi kwenye vyama vya michezo ngazi ya taifa hadi vile vya wilaya.
Wizara kwa nafasi yake inashindwa kutekeleza majukumu yake katika sekta ya michezo. Inachokifanya ni kuongoza michezo kwa mazoea kwa viongozi wake kukaa ofisini na kusubiri ripoti.
Vivyo hivyo, BMT inaongoza sekta hiyo kwa mazoea pia kama vilivyo vyama vya michezo ambavyo viongozi wake wapo ili mradi wanaitwa viongozi, lakini hawatambui majukumu yao ni yapi katika sekta hiyo.
Mifumo ya uendeshaji michezo ipo, lakini haizingatiwi. RT imeshindwa kupeleka wanariadha kwenye mashindano ya Afrika, tunaona ni kawaida hakuna wa kuhoji. Hali ni kama hiyo BFT.
Kwenye vyama vya mikoa na wilaya pia hakuna kinachotendeka zaidi ya ubabaishaji. Hali ya viongozi wetu wa michezo inanipa shaka, Watanzania wamepiga kelele, wameshauri na hata kutoa madukuduku yao bila mafanikio labda tujaribu njia ya maombi. Lakini ni vema viongozi wetu wa michezo watangazwe kuwa ni janga kwa viongozi hawa huenda wakabadirika. Maoni 0756 667 666

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga