Viongozi wa riadha Tanzania wakubali makosa

Tulitegemea Shirikisho la Riadha la Taifa (RT) lingeyatumia mashindano hayo kuanza kutengeneza timu ya ushindani ambayo itashiriki kwenye Michezo ya Afrika mwakani.PICHA|MAKTABA 
Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) limeshindwa kupeleka wanamichezo kwenye mashindano ya Afrika ya riadha yaliyomalizika wiki iliyopita jijini Marrakech, Morocco na kushirikisha wanariadha 600 kutoka mataifa 47.
Mashindano hayo yalifanyika kwa siku nne, kuanzia Agosti 10 mpaka 14 huku Afrika Kusini ikiongoza kwa kutwaa medali nyingi, ikifuatiwa na Nigeria na Kenya.
Katika mashindano hayo, Zanzibar ilipeleka wanariadha wawili waliochuana katika michezo ya kurusha kisahani, mkuki na tufe huku Bara ikishindwa kupeleka mkimbiaji hata mmoja. Kitendo cha Bara kushindwa kupeleka wanamichezo katika mashindano hayo ya riadha ya Afrika kimewanyima fursa wanariadha kwenda kushindana na kutafuta viwango vitakavyowasaidia kwenye mashindano mengine ya kimataifa.
Mashindano hiyo ya riadha ni moja ya mashindano makubwa kwa nchi za Afrika ambayo, ukiondoa Michezo ya Afrika, huenda ikawa ya pili kwa ukubwa. Michezo hiyo hushirikisha wanariadha wenye viwango vizuri. Tulitegemea Shirikisho la Riadha la Taifa (RT) lingeyatumia mashindano hayo kuanza kutengeneza timu ya ushindani ambayo itashiriki kwenye Michezo ya Afrika mwakani.
Hii ni kwa sababu, kwa kushiriki kwenye mashindano hayo ya riadha, wanariadha wa Tanzania wangebaini uwezo na viwango vyao kabla ya Michezo ya Afrika ambayo ni kama Olimpiki ya bara hili kutokana na ukweli kuwa hushirikisha michezo tofauti.
Tunakumbuka RT iliwaweka kambini wanariadha wengi kwa ajili ya kujiandaa na Michezo ya Jumuiya ya Madola ya msimu huu na baadhi yao walishiriki michezo hiyo na wengine waliachwa. Pia kwa kuwa RT ilifanya mashindano ya taifa katikati ya mwaka huu jijini Dar es Salaam, ingetoa nafasi kwa wanariadha waliofanya vizuri wangekuw awamekata tiketi ya kushiriki katika Mashindano ya Riadha ya Afrika.
Tunajua viongozi wa RT wanaweza kujitetea kuwa hao wanariadha wawili wa Zanzibar waliokwenda Morocco waliiwakilisha Tanzania kwa ujumla, lakini kwenye mashindano makubwa kama yale taifa halikustahili kupeleka wanariadha wawili tu kwani Tanzania ina wanariadha wengi tu.
Sisi tunaamini RT ilitakiwa kupeleka wanariadha wengi katika mashindano hayo makubwa ya riadha barani Afrika kwa kuwa yangewasaidia kuwapa mwanga na kuwandaa kwa michezo ijayo. Mara kwa mara tumekuwa tukiwakumbusha viongozi wa vyama vya michezo nchini kutimiza wajibu wao wa kuendeleza michezo, lakini katika hali ya kushangaza hilo limekuwa likishindikana.

Viongozi wa RT wameendelea kufanya mambo kwa mazoea na hakuna wa kuwauliza, tunajidanganya kwamba ipo siku tutafanya vizuri kwenye mashindano ya kimataifa kwa aina hii ya viongozi wa michezo tulionao.
Sisi tunaamini kuna uzembe mkubwa unafanywa na RT na hatutakiwi kuufumbia macho kwani tunavyozidi kuchelewa kukemea ndivyo tunavyozidi kujimaliza katika mchezo wa riadha ambao tulikuwa tukifanya vizuri miaka ya nyuma.
Kitendo cha RT kushindwa kupeleka wanariadha katika mashindano hayo ni dalili kwamba tumekubali kuua mchezo wa riadha nchini, tumekubali kujipoteza kimataifa na tumekubali aibu. Viongozi wa RT wakubali wamekosea na hivyo kutafuta sababu za kukosea na kurekebisha.

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga