Wawakilishi Madola wameifedhehesha nchi

Julai 16, Rais Jakaya Kikwete alimkabidhi Bendera ya Taifa nahodha wa Tanzania katika Michezo ya Jumuiya ya Madola, Seleman Kidunda kwa matumani kwamba timu itaipeperusha vyema kwenye michezo hiyo ya 20 iliyofanyika kwenye jiji la Glasgow, Scotland.
Rais alifika Uwanja wa Taifa kwa kazi hiyo, akiwa na matumaini ya vijana wake kuwa watalinda heshima ya nchi katika michezo hiyo mikubwa iliyoshirikisha mataifa 71. Kinyume na matarajio hayo, matokeo ndivyo kama yalivyosikika na kuonekana. Tanzania haikuambulia hata medali moja katika michezo hiyo ya Madola kama ilivyokuwa kwenye michezo ya 19 iliyofanyika New Delhi, India mwaka 2010.
Katika michezo hii, tunautazama ushiriki wa Tanzania katika maeneo mawili; maandalizi na ushiriki wa timu zake saba za riadha, ngumi, kuogelea, mpira wa meza, judo, kunyanyua vitu vizito na baiskeli.
Katika maandalizi, hakuna ubishi kuwa Tanzania ilivurunda. Viongozi waliosindikiza timu kwenye michezo ya Madola pamoja na watu wengine, hawakumwambia Rais Kikwete ukweli wa hali halisi wa timu zetu.
Wizara ilimpa Rais Kikwete jukumu la kukabidhi bendera ya Taifa kwa wanamichezo na viongozi waliokwenda kwenye michezo hiyo, kumbe hakukuwa na ukweli na undani wa uimara wa wanamichezo na maandalizi yake.
Wanariadha walishindwa kirahisi, mabondia walipigwa kirahisi na mbaya zaidi kwa mabondia wa Tanzania kusimamiwa na makocha wa Kenya katika michezo hiyo. Kama kocha aliyemfundisha bondia hana kiwango, yule anayefundishwa atafaulu? Hivi kweli, kwa staili hii kulikuwa na dalili za medali? Ilielezwa kuwa makocha wa Tanzania hawakuwa na sifa za kufundisha mabondia wa michezo hiyo. Kweli hapo tulitegemea medali na kumpa Rais jukumu la kukabidhi Bendera ya Taifa? Pia tuliambiwa mmoja wa mabondia wetu aliumwa tumbo na akashindwa kupanda ulingoni na pia ilielezwa kuwa kuna kocha mmoja alikuwa na kidonda na kushindwa kufanya kazi yake barabara.
Hivi kabla ya timu kuondoka, hayo yote yalikuwa hayafahamiki? Wakati Rais anakabidhi bendera, wangemwambia tu kuwa tunakwenda, lakini maandalizi yetu si ya kuleta medali pamoja na kwamba mmetuweka kambini nje ya nchi miezi miwili, tofauti na sasa wanatoa visingizio baada ya kurejea.
Ni vyema basi wangemtuma tu mwakilishi wa wizara kwa ajili ya kukabidhi bendera kuliko kumualika Rais huku wakijua kulikuwa na kashfa ya uwezo wa ushiriki wa wanamichezo wetu.
Tunaamini kuwa Serikali itataka taarifa ya kina kuhusu ushiriki wa timu zetu kwenye mashindano hayo, ambayo itaeleza kwa undani sababu za timu zetu kutofanya vizuri, baadhi ya wanamichezo kushindwa kutokea jukwaani na masuala mengine yatakayosaidia kusahihisha pale tulipokosea na kuadhibu pale palipokuwa na uzembe.

Zaidi ya hayo, tunajua kuwa kuna kashfa hii ya matumizi ya fedha ambayo hadi sasa bado haijatolewa ufafanuzi wa kutosha. Tunaamini katika mashindano kama haya makubwa, timu hupewa malazi kwenye kijiji maalum cha wanamichezo. Hivyo, kiongozi wa msafara hana budi kutoa taarifa ya nini kililipiwa na Serikali na nini kililipiwa na waandaaji ili kuondoa hisia za ufisadi katika Dola 93,000 zilizotolewa na kampuni ya SS Bakhresa kwa wanamichezo.
Tunadhani, ifike hatua viongozi na makocha wawe wawazi pia vyama viwajibike kwa matokeo mabaya ambayo timu zake zinakuwa zinapata kwenye mashindano ya kimataifa kama zitashindwa kuandaa timu mapema. Wachezaji wasishiriki mashindano ya kimataifa ili mradi bali timu ziwe zimeiva na hata ikitokea tumeshindwa ionekane kweli tulipambana kuliko ilivyo.Ukweli, viongozi na wasimamizi wa timu za Tanzania zilizoshiriki Madola wamemfedhehesha Rais. Kwa hayo yaliyotokea, wanatakiwa wamtake radhi, kiungwana.

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga