Kwa mwenendo huu, michezo haitafanikiwa Tanzania

Mama Anna Kibira / Mwenyekiti wa Chama cha Netboli Taifa(CHANETA)
Kuondolewa kwa timu ya taifa ya netiboli kwenye harakati za kutafuta tiketi ya kufuzu kushiriki fainali za Kombe la Dunia ni mwendelezo wa matukio ya kusikitisha yanayoendelea kuzikumba timu za taifa za Tanzania.
Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta) kilitangaza kuiondoa timu hiyo kutokana na kukosa fedha za gabarone, Botswana kushiriki mashindano ya Afrika ya kutafuta tiketi ya kwenda Kombe la Dunia.
Huenda kwa mara ya kwanza tungeshuhudia Taifa Queens ikikata tiketi ya kushiriki michuano hiyo mikubwa, lakini ndoto hizo ziliyeyushwa na Chaneta.
Chaneta ilitembeza bakuli la kutafuta fedha za kufanikisha safari hiyo, lakini haikufanikiwa. Kushindwa kwa Taifa Queens kwenda kwenye mashindano hayo ni mwendelezo wa timu za Taifa kukosa mashindano muhimu.
Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) pia limekuwa likijiendesha kwa mtindo huo, hali kadhalika kwa vyama vya ngumi, kikapu, mpira wa meza, judo na vingine vingi. Utaratibu huo wa kutembeza bakuli unaotumiwa na vyama umekuwa ukididimiza michezo yetu kimataifa na waathirika wakubwa katika hilo wakiwa wachezaji.
Tumekuwa tukishuhudia mataifa mengine yakipata mafanikio katika sekta ya michezo siyo kwa kutumia mtindo wa kutembeza bakuli bali mifumo mizuri ya udhamini na vyanzo vya uhakika vya mapato. Hapa nchini ni dhahiri Serikali imejiondoa kusaidia michezo, kwani hutenga fedha kidogo sana katika bajeti ya maendeleo ya michezo, pia hutoa mchango mdogo kwa timu za taifa.
Matukio ya timu za taifa kujiondoa kwenye mashindano ya kimataifa yamekuwa ya kawaida, hakuna anayehoji wala anayetafakari ni kiasi gani Tanzania inazidi kupoteza dira katika nyanja ya michezo kimataifa.
Kila siku sera za viongozi wa vyama na mashirikisho haya ya michezo ni kulalamika. Hakuna chama wala shirikisho lenye afadhali kimapato ambalo linaweza kujiendesha.
Asilimia 95 ya vyama na mashirikisho ya michezo hapa nchini hayana vyanzo vyake vya mapato vya kueleweka. Karibu vyote vinajiendesha kwa kutembeza bakuli. Mtindo huu umekuwa ukididimiza maendeleo ya michezo kwani timu ya taifa ya ngumi ilikwama kushiriki kwenye mashindano ya Afrika nchini Morocco, pia riadha nayo ilikwama kabla ya netiboli kukwama baada ya vyama vya michezo hiyo kutembeza bakuli bila mafanikio.

Tabia hii ya kutembeza bakuli imeanza kuigharimu Tanzania kwani tumeshuhudia timu ya netiboli ikizidi kuporomoka na sasa imezidiwa hadi na Uganda kwenye viwango vya kimataifa. Serikali ilipojitoa kusaidia michezo moja kwa moja, nilitegemea wangeiacha katika misingi mizuri ya kujiendesha, lakini cha kushangaza utaratibu wa michezo uliotumika miaka 30 iliyopita ulikuwa bora kushinda sasa.
Niliwahi kuzungumza na baadhi ya wanamichezo wa zamani ambao walionyesha kustaajabu mfumo hasi unaotumika hivi sasa kulinganisha na miaka ya 70 mpaka 80. Wanamichezo hao wa zamani waliniambia Taifa halikuwa na utaratibu wa kutembeza bakuli. Michezo iliwekwa katika bajeti za Serikali na mafanikio yalionekana ambayo hivi sasa yamebaki historia.
Hakuna njia ya mkato ya kufanikiwa katika michezo bali ni vyama kuwa na vyanzo vyake vya mapato au udhamini wa kudumu kwa timu zao, ikiwezekana Serikali kuingilia kati.
Kwa mtindo huu wa kutembeza bakuli hatuwezi kufanikiwa katika sekta ya michezo kimataifa zaidi ya kuwa wasindikizaji. Mwandishi wa uchambuzi huu ni mwandishi wa habari wa habari wa gazeti hili.

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga