Tathmini ya Madola, ifanyiwe kazi

Timu ya Tanzania kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola yakaribishwa rasmi leo katika kijiji maalum cha michezo hiyo Glasgow
Kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, Serikali ilikutana na wanamichezo kwa ajili ya kufanya tathmini ya ushiriki wa taifa kwenye michezo ya Jumuiya ya Madola ya 2014 ambayo Tanzania ilitoka kapa kwa mara ya pili mfululizo.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ndiye alikuwa mgeni rasmi katika tathmini hiyo iliyowahusisha wachezaji, makocha na viongozi wa vyama mbalimbali vya michezo.
Katika tathmini hiyo, vyama vililalamikiwa kutokuwa makini katika kuziandaa timu zao kwa ajili ya mashindano ya kimataifa.
Maandalizi duni ilikuwa ni moja ya sababu kubwa iliyotajwa katika tathmini hiyo iliyohusisha wanamichezo wa ngumi, riadha, mpira wa meza, judo, kuogelea, baiskeli na kunyanyua vitu vizito walioiwakilisha nchi katika michezo ya madola iliyofanyika Scotland.
Maandalizi ya zimamoto ni ugonjwa sugu ulio kwenye timu za Tanzania, baada ya tathmini ya madola nilitegemea vyama vingeanza kujipanga na kujiandaa kwa ajili ya michezo ya Afrika ya 2015.
Baada ya tathmini ile kila chama kimeshika njia yake, hakuna kinachokumbuka kufanya maandalizi ya kina kama ambavyo vilieleza katika tathmini ya Madola.
Mataifa ya Afrika yanayofanya vizuri katika michezo tayari yameanza maandalizi kwa ajili ya michezo ya Afrika, tofauti na Tanzania ambayo imekuwa na rekodi mbaya kwenye michezo kimataifa na hakuna chama kinachokumbuka maandalizi.
Licha ya kwamba Waziri Membe aliahidi kufanya jitihada kuhakikisha aibu ya madola haijirudii kwenye michezo ya Afrika, bado jitihada hizo zinapaswa kuungwa mkono na vyama vya michezo. Baada ya kumalizika michezo ya Madola nilitegemea vyama vingejifunza kutokana na makosa, vingetambua umuhimu wa mazoezi hatua baada ya hatua na mchakato hadi mchezaji kushinda medali.
Imekuwa kinyume, vyama sasa viko likizo vinaona 2015 ni mbali, vimekaa vikisubiri miezi miwili kabla ya mashindano ndipo vianze maandalizi. Imefikia hatua sasa Watanzania wamezichoka timu zao, wanapoteza imani nazo kila zinapokuwa kwenye mashindano ya kimataifa.
Ubabaishaji wa viongozi wetu wa michezo ndiyo chanzo, viongozi wetu wanapenda mtelemko katika maandalizi.
Tulishuhudia wakati timu zikichaguliwa kwenda kwenye kambi nje ya nchi iliyoandaliwa na serikali kabla ya michezo ya madola kufanyika, viongozi wa vyama walikuwa mstari wa mbele kuchuja wachezaji na kujipendekeza kuwa makocha.

Japo wamekuwa wa mwisho kuweka mikakati ya kutafuta fedha kwa ajili ya kuziandaa kwa kina timu zao ili kuhakikisha zinafanya vizuri kimataifa. Tena cha kushangaza hao hao viongozi waliofanya kampeni kisha kupigiwa kura ili kuongoza vyama na mashirikisho yetu ya michezo ndiyo wanakuwa mstari wa mbele kusema maandalizi hayakuwa mazuri.
Kama kiongozi anasema maandalizi hayakuwa mazuri alitegemea muujiza gani ushuke kwa ajili ya kuratibu maandalizi ya wanamichezo wa chama anachokiongoza?. Kama vyama vya michezo vikishindwa kubadilisha mifumo yao ya maandalizi kwa wanamichezo hakuna shaka hata kwenye michezo ya Afrika 2015 hali itakuwa ileile kwa Tanzania.
Kama kweli Taifa linahitaji mafanikio, viongozi wa vyama vya michezo wangezifanyia kazi kasoro zote zilizoainishwa na wachezaji wakati wa ufanyaji tathmini vinginevyo taifa litaendelea kutwanga maji kwenye kinu katika michezo kimataifa.
Mwandishi wa uchambuzi huu ni mwandishi wa habari wa gazeti hili.

CHANZO: Mwananchi

Comments

Popular

GIDABUDAY KUHAMASISHA UJENZI WA KIJIJI CHA MICHEZO TANZANIA LENYE JINA YA MWANARIADHA MKONGWE BW.JOHN STEPHEN AKHWARI

Rio Olympics: Brazil win men's volleyball gold, GB's Joyce takes boxing silver – as it happened

Olympics 2016: Usain Bolt completes sprint double, Jade Jones retains taekwondo title

Rio Olympics: Swimmer Lochte apologises for 'robbery' saga